Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) Wilaya ya Tandahimba umetenga Shilingi 452,500,000 kwa ajili ya kuchimba visima vitano vya maji safi na salama katika vijiji vya Mivanga, Lyenje, Dinduma, Mchangani na Michenjele, kwa lengo la kuondoa kero ya muda mrefu ya upatikanaji wa maji kwa wakazi wa maeneo hayo. Akizungumza wakati wa utoaji wa taarifa ya utekelezaji wa mradi huo kwa Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa mwaka 2025, Ismail Ali Ussi, Meneja wa RUWASA Wilaya ya Tandahimba, Falaura Kikusa alisema kuwa mradi huo ni sehemu ya Programu Maalumu ya Serikali chini ya Rais Samia Suluhu Hassan inayolenga kuhakikisha wananchi wote wanapata huduma ya majisafi na salama. “Mradi huu ni mkakati maalumu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa lengo la kupunguza adha ya maji katika maeneo ambayo hayajafikiwa na huduma hii muhimu. Utekelezaji wake ulianza Mei 2024 na unatarajiwa kukamilika Juni 2025 kutokana na changamoto mbalimbali, licha ya mpango wa awali kumali...